Monday, June 6, 2011

MAPACHA WATATU MSIJE KUWA NDUMILA KUWILI KAMA WALIOWATUNGULIA KUZIKIMBIA BENDI ZAO

MAPACHA WATATU: Haturudi nyuma kamwe  Send to a friend
Saturday, 30 April 2011 20:37
0diggsdigg

Na Furaha Maugo
NI kundi linalofanya vizuri katika medani ya muziki wa dansi hapa nchini kwa sasa, linaundwa na vijana watatu ambao hawajazaliwa na baba wala mama mmoja, lakini bado wanajiita mapacha watatu.
Wakali hao ambao awali kabla ya kuunda kundi hilo, walikuwa katika bendi mbili tofauti za muziki wa dansi hapa nchini, hivi sasa wamekuwa gumzo katika anga la starehe na hasa muziki wa dansi.
Uwezo wao pia umedhihirika baada ya kujinyakulia tuzo ya wimbo bora wa Kiswahili wa mwaka katika tuzo za kili Music Awards 2010/11, ikiwa ni muda mfupi tu tangu kuanzishwa kwa kundi hilo na kuyabwaga makundi nguli wa muziki wa dansi kama Extra Bongo, Twanga Pepeta na Akudo Impact.
Awali kundi hili lilikuwa likiwatumikia mabwana wawili kwa wakati mmoja; walikuwa wakiimba katika bendi zao na pia kulitumikia kundi lao ambapo Josee Mara alikuwa kundi la FM Academia, na Chokoraa na Kalala Jr walikuwa Twanga Pepeta.
Lakini ndoa hiyo iliwashinda na kuamua kuachana na bendi zao, ni hivi karibuni, Meneja wa wakali hao, Hamis Dakota amesema kuwa wanamuziki wake hawafikirii kurudi nyuma tena.
Dakota alisema kundi lake limejipanga vizuri kuhakikisha wanakabilia na soko la ushindani lililopo sasa na wanaamini watafanya vizuri kwa sababu imezungukwa na vichwa vikali katika tasnia ya muziki wa dansi.
“Kiukweli sasa hivi tunataka mabadiliko ikiwa ni pamoja na kuwa na  nyumba nzuri ya kuishi na maisha mazuri na haya yote yataletwa ikiwa tutafanya  kazi kwa juhudi na maarifa kila kukicha kwa ubunifu wa hali ya juu” anasema Dakota.
 “Mashabiki wakao mkao wa kula kwani tayari albamu ya pili yenye  jumla ya nyumba sita  imeshakamilika japokuwa hatujaipa jina rasmi ” anaongeza kusema Meneja Dakota.
Baadhi ya nyimbo zitakazokuwepo katika Albamu hiyo ni pamoja na Mjasiriamali iliyoimbwa na kutungwa na Chokoraa, Usia wa babu ya  Josee Mara, Mtoto wa Paka ya  Kalala junior, Sumu ya mapenzi remix ya Kalala Jr na Gari bovu ulioimbwa na kutungwa na mpiga vyombo Arosto Mashama .
Mapacha watatu walifikia uamuzi wa kuunda kundi lao mwaka 2010, vijana hao ambao wamekulia katika muziki na wamepitia bendi kubwa hapa nchini, haikuwapa shida kuwateka mashabiki wa muziki wa dansi kwani tayari walikuwa wakipendwa hata huko walipokuwa kabla ya kuunda kundi lao wenyewe.
Baada ya kuunda kundi la Mapacha Watatu, waliendelea kufanya shughuli zao kote kote, wakiimba na kufanya maonesho mbalimbali wakiwa na bendi zao (Twanga na FM Academia), huku pia wakilazimika kutumia nguvu zaidi kufanya maonyesho ya bendi yao.
Baada ya muda mfupi walifanikiwa kuachia Albamu yao ya kwanza iliyopewa jina la ‘Jasho la Mtu’ na ilikuwa na nyimbo kama ‘Shika ushikapo’, ‘Kipaji Changu’ na ‘Muhudumu’ wimbo ulio na mahadhi ya Afrika Magharibi (Gauo) ziliweza kufanya vizuri .
Ni kutokana na umahiri wao katika muziki wa dansi, wimbo wa ‘Shika Ishikapo’ uliweza kupendwa na hadi kuchaguliwa kuwa wimbo bora wa Kiswahili kwa mwaka 2010/11 katika tuzo za muziki za Kili, huku Khalid Chokoraa akishinda tuzo ya Rapa bora wa Kiume wa mwaka 2010/11 katika tuzo hizo.

No comments:

Post a Comment