Tuesday, March 22, 2011

SAKATA LA WAZIRI MAGUFURI NA SERIKARI LAENDELEA

JK naye 'ampiga kufuli' Magufuli  Send to a friend
Monday, 21 March 2011 21:14
0diggsdigg
Sadick Mtulya na Gedius Rwiza
RAIS Jakaya Kikwete amemuagiza Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli kuzingatia utu pamoja na historia ya eneo husika wakati wa utekelezaji wa bomoabomoa kwenye hifadhi ya barabara nchi nzima.Pia, amemuagiza Dk Magufuli kuwalipa wote wanaostahili fidia na kwamba wasiangalie tu mazingira ambayo yataepusha mzigo wa gharama kwa Serikali.Kauli hiyo ya Rais Kikwete imekuja siku chache baada Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kusimamisha bomoabomoa hiyo mpaka shauri hilo litakapoamuliwa vinginevyo na Baraza la Mawaziri.

Rais Kikwete alisema hayo jana baada ya Dk Magufuli kumuomba Rais Kikwete ampe ruhusa ya kuendelea na ubomoaji huo. Jana, Rais alikutana na watendaji wa Wizara ya Ujenzi katika mfululizo wa ziara zake za kukagua utekelezaji wa maagizo yake.
"Mheshimiwa Rais, niliapa kulinda sheria na Katiba ya nchi, hivyo ninaomba nipewe ruhusa kutekeleza sheria ya kubomoa nyumba zilizojengwa ndani ya hifadhi ya barabara,'' alisema Dk Magufuli.Waziri Magufuli amekuwa akisisitiza kwamba waliojenga ndani ya barabara wamevunja Sheria namba 13 ya mwaka 2007 na kwamba hawastahili kulipwa fidia.
Hata hivyo, Rais Kikwete akijibu maombi hayo alisema: ''Hili naliongea kwa umakini kwani nataka nieleweke vizuri. Bomoabomoa ipo. Usilegee katika kutekeleza sheria, lakini uangalie ubinadamu katika bomoa hiyo pamoja na historia ya eneo husika. Pia muwalipe wote wanaostahiki kulipwa fidia na msiwalipe wale wasiostahiki na msiangalie unafuu wa Serikali pekee.''
Rais Kikwete alisema itakuwa ni jambo la kushangaza endapo hata vitu vya kihistoria, ikiwamo nyumba na sanaa mbalimbali ambazo zimejengwa katika hifadhi ya barabara zitabolewa.Kuhusu utu, alisema kulingana na ubinadamu, kubomoa nyumba ambayo imejengwa na kukaliwa kwa muda mrefu harakaharaka itakuwa ni kinyume na haki za binadamu... "Ikifikia hatua ni lazima nyumba hiyo ibomolewe, toeni muda wa kutosha ili wajiandae kwani kuwatoa kwa haraka itakuwa ni kinyume na haki za binadamu.
Hata hivyo, Rais Kikwete aliagiza iundwe tume maalumu na ya kudumu itakayokuwa ikifuatilia hifadhi za barabara nchini kote akiwaagiza watendaji wa wizara hiyo kuwa wakali katika kusimamia fedha za miradi ya barabara na kuwataka wasiwaonee haya wanaosababisha kutokamilika au miradi kutekelezwa kinyume na makubaliano.
"Pamoja na mambo mengine, endeleeni kutupia macho ya umakini. Rushwa imezidi na inasababisha kuharibika kwa barabara kutokana na kupitishwa kwa mizigo mizito kinyume na utaratibu,'' alisema.

Pinda alichomwambia Magufuli Chato
Machi 6, mwaka huu akihutubia wananchi katika mkutano wa hadhara mjini Chato, mkoani Kagera, Waziri Mkuu Pinda pamoja na kumsifu Dk Magufuli kwa utendaji wake, alimwagiza kusimamisha bomoabomoa zote hadi hapo Serikali itakaposema vinginevyo.
Tamko la Pinda lilitokana na hatua aliyoichukua Dk Magufuli Januari 13, mwaka huu ya kutoa ilani kwa wananchi waliojenga nyumba ndani ya hifadhi ya barabara kuanza kubomoa nyumba hizo mapema na kwamba wasitegemee kulipwa fidia.Dk Magufuli pia alimtaka Meya wa Jiji la Dar es Salaam pamoja na madiwani kujipanga na kuondoa nyumba zilizo katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya njia ya mabasi yaendayo kasi ili kuwawezesha makandarasi kuanza kazi hiyo.
Pinda alisema kasi aliyoanza nayo Magufuli katika wizara yake mpya imeitisha Serikali... “Rais aliona kwenye barabara panalegalega na kumrudisha Magufuli kwenye wizara hiyo. Huyu Serikalini tunamwita ‘buldoza’ hata hivyo, ameanza kwa speed (kasi) kubwa na tumwemwagiza asimamishe zoezi hilo mpaka litakapojadiliwa na Baraza la Mawaziri.”
Alisema baraza hilo litafanya kikao ili kuangalia upya maeneo yaliyopangwa kwa ajili ya bomoabomoa na kusema kuwa kabla ya kuruhusu kuendelea lazima wakubaliane kwanza kwenye Baraza la Mawaziri, pamoja na kutolewa elimu kwanza na akasema kuwa katika maeneo mengine bomoabomoa si lazima.
Alisema bomoabomoa hiyo ambayo imezua malalamiko imesimamishwa na Serikali kwa nia ya kujipanga upya, huku akisisitiza kuwa Serikali inamwamini Waziri Magufuli kama kiongozi mwenye uwezo na ilimpa nafasi hiyo ili pia aweze kuwabana makandarasi wazembe.
Kasi hiyo ya Dk Magufuli imeyakumba majengo kadhaa ya Serikali, likiwapo la Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Dar es Salaam na jengo la Makao Makuu ya Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (Tanesco).
Hata hivyo, baadhi ya wakazi wanaoishi kandokando ya Barabara ya Ubungo Maziwa hadi Kigogo, wamefungua kesi mahakamani kupinga kubomolewa bila fidia.

JK akerwa na maofisa ardhi wala rushwa
Jana akiwa katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi, Rais Kikwete amewataka watendaji wake kuwachukulia hatua maofisa ardhi wanaojihusisha na vitendo vya rushwa akisema wamekuwa chanzo cha migogoro ya ardhi.
“Wizara inatakiwa kuwachukulia hatua maofisa ardhi wote wanaojihusisha na vitendo vya rushwa huku wakidiriki kuuza maeneo ya wazi na kuwadhulumu wananchi.
Hakuna kumwonea mtu huruma maana wananchi wanaonewa,” alisema Rais Kikwete. Alisema hata malipo ya fidia yanatakiwa kuendana na hali halisi ya maisha na siyo kumhamisha mtu bila kumwandalia makazi ya kudumu... “Huwezi kumhamisha mtu bila kumwandalia makazi ya kudumu yanayoendana na hali ya maisha ya sasa, vinginevyo hakuna haja ya kumwondoa katika makazi yake.
Tunatakiwa kutumia ubinadamu.” Aliitaka Wizara kuorodhesha halmashauri zinazoongoza kwa migogoro ya ardhi ili kuona chanzo cha migogoro na kuwachukulia hatua maofisa wote wa ardhi wanaokiuka taratibu.Pia alilitaka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kupunguza gharama za kodi kwenye nyumba zake na kuhakikisha majengo yao yanaboreshwa ili wanaopanga katika nyumba hizo waishi katika hali ya usafi.
“Ukweli ni kwamba gharama zenu zinatisha mtu wa kawaida. Mwenye kipato cha chini hawezi kupanga nyumba zenu. Mnatakiwa kupunguza gharama hizo ili kuwawezesha wananchi kumudu gharama hizo vinginevyo wengi watazikimbia,” alisema Rais Kikwete.

No comments:

Post a Comment