Monday, May 16, 2011

JE KUNA UHUSIANO KATI YA UFAULU WA WANAFUNZI NA UPATIKANAJI WA CHAKULA MASHULENI?

Weekend imeenda pouwa sana mtu mzima kwizera! kuhusu mada inayohusanisha chakula na ufaulu wa wanafunzi mashuleni,ni kweli kuna uhusiano mkubwa kati ya ufaulu wa wanafunzi na chakula,vijijini mara nyingi vyakula huwepo kwa wingi wakati wa mavuno lakini msimu wa mavuno ukishapita wanakijiji wengi hukubwa na tatizo la chakula kwa kuwa hawana elimu ya uhifadhi wa chakula,lakini pia mafuno wanakijiji wanayopata hayawawezeshi kufikia msimu mwingine wa mavuno. Hivyo,sehemu nyingi za vijijini wanafunzi wanafunzi hukubwa na njaa,mwanafunzi mwenye njaa hukosa hamasa ya kujifunza kwa bidii kwa kuwa muda mwingi watakuwa wanfikiria namna ya kukabili njaa inayowakumba badala ya kufuatilia yale wanayofundishwa na walimu mashuleni.Ndugu yangu Kwizera mimi mwenyewe ni mhanga wa kutokufaulu vizuri mitihani yangu ya primary school kwa tatizo la njaa,nakumbuka mimi na wenzangu tulikuwa tunakabiri njaa zetu kwa kwenda kuwasidia wafanya biashara kusukuma baiskeli zao zilizobeba mizigo kupanda mlima RUSUNWE wilayani KASULU kuelekea Burundi,na kisha kupatiwa fedha kiduchu ambazo tuliweza kunnua chakula, hali hiyo ilituathiri sana kitaaluma kwa kuwa kazi za kusukuma baiskeli kupanda mlima RUSUNWE tulikuwa tunaifanya wakati wa masomo. Hali hiyo ingeweza kuzuwilika kama tungekuwa tunapewa chakula mashuleni maana tungeelekeza mawazo yetu na fikira zetu katika masomo badala ya kuelekeza mawazo yetu na fikra zetu katika kusukuma baiskeli kupandisha mlima RUSUNWE ili kupata fedha za kununulia chakula.
Hivyo kama kutakuwapo mpango unaotekelezeka wa kuwapatia wanafunzi wa shule zetu za msingi chakula walau cha mchana,licha ya kuongeza ufaulu wa wanafunzi lakini pia mpango wa chakula mashuleni utaweza kuongeza mahudhurio ya wanafunzi mashuleni,kupunguza utoro reja reja wa wanafunzi mashuleni na kuongeza molari za wanafunzi kujifunza na kufuatilia kile wanachofundishwa madarasani.
Mimi ni LEONARD KILAMHAMA

JE NI KWELI NCHI HAITAWALIKI?


Dk. Slaa:
[Image] KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk.Willbrod Slaa, sasa ametamka rasmi kwamba nchi haitatawalika, kwani chama chake hakiko tayari kuona Watanzania wakiendelea kuwa katika hali ngumu ya maisha, huku Chama cha Mapinduzi (CCM) kikitekeleza mkakati wa siri wa kuwajaza matumaini hewa badala ya kutatua matatizo yao.
Dk. Slaa ameeleza kuunasa waraka wa siri wa CCM ambao ndani yake chama hicho kimekiri waziwazi kupoteza ladha kwa umma, huku mkakati pekee wa kujinusuru ukielezwa kuwa ni kubadili sura za viongozi wa chama hicho ili kuwajengea matumaini mapya Watanzania.
Kwa mujibu wa Dk.Slaa, waraka huo wenye mhuri mkubwa wa neno “siri” uliandaliwa na baadhi ya wataalam wa CCM waliofanya tathmini ya hali ya chama chao kisiasa na kuuwasilisha kwa viongozi wa juu wa chama hicho ambao tayari wameanza kuufanyia utekelezaji wa “kujivua gamba” kwa lengo la kuwapa matumaini hewa wananchi.
Dk. Slaa alifichua siri za waraka huo wakati akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara katika viwanja wa shule ya sekondari Msakila mjini Sumbawanga ikiwa ni siku ya kwanza ya ziara ya chama hicho mkoani Rukwa, baada ya kuutikisa mkoa wa Mbeya kwa maandamano na mikutano ya hadhara kwa siku tatu mfululizo.
Alisema katika waraka huo CCM imekiri kuwa haikubaliki kwa Watanzania na kwamba iliporomoka sana katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana, lakini badala ya kurejesha tunu za taifa kama uadilifu, upendo, amani, umoja na uwajibikaji wa kuleta maendeleo yatakayoirejeshea imani toka kwa wananchi, chama hicho kimeamua kubadili tu sura za viongozi wake wa kitaifa.
“CHADEMA tunafanya mambo kwa utafiti. CCM wana waraka wa siri uliowafanya wajivue gamba lakini wanaume tayari tumeshaunasa, tena una mhuri mkubwa wa neno siri lakini tayari tunao. Katika waraka wao CCM wamekiri wenyewe kwamba hawakubaliki tena kwa Watanzania walio wengi, wamekiri wenyewe kwamba wamepoteza ladha kwa wananchi. Wamekiri wenyewe katika waraka huo, kwamba hawakubaliki kwa sababu wameacha siasa ya ujamaa na kujitegemea.
“Na ni kweli wameacha siasa ya ujamaa na kujitegemea. Mabilioni ya Kikwete sio ujamaa na kujitegemea. Mabilioni ya mtoto wake, anayeitwa Ridhawani nayo ni ushahidi tosha kuwa wameacha ujamaa na kujitegemea kama walivyokiri wenyewe kwenye waraka wao.
“Tatizo lao ni kwamba badala ya kuacha ufisadi na kurejesha tunu za taifa kama uadilifu, upendo, amani, umoja na uwajibikaji…badala ya kupunguza kodi kwenye mafuta, sukari, saruji, na bidhaa nyingine, ili wajijengee uhalali kwa umma, wao katika waraka wao wameamua wabadili sura za viongozi kwa kujivua gamba. Hawataji popote kwenye waraka wao jinsi watakavyoboresha maisha yenu,” alisema Dk.Slaa na kuongeza.
“CHADEMA hatuko tayari kuona Watanzania wakiteseka huku CCM yenye serikali badala ya kuchukua hatua za dharura kuwanusuru, inapanga kuendelea kuwadanganya kwa kubadili viongozi kwa kujivua gamba. Arusha nilitoa hotuba moja wakasema Dk. Slaa mchochezi…sasa leo nawatuma usalama wa taifa nendeni mkawaambie CCM kwamba nchi haitatawalika. Wasipochukua hatua CHADEMA itachukua hatua…kama Watanzania hawajui wanakula nini, wanavaa nini, watoto wao wanasoma vipi, wanatibiwa vipi, basi nchi hii haitatawalika.”
Alisisitiza kuwa nchi haitatawalika kwani kila kukicha ufisadi unakithiri badala ya kupungua huku akibainisha kuwa hata ripoti ya mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu za serikali ya hivi karibuni imeonyesha katika wizara moja pekee, wizara ya fedha na uchumi, jumla ya sh bilioni 365 ziliibiwa wakati zingeweza kutumika kunusuru maisha ya Watanzania.
Mwenyekiti wa chama hicho akihutubia wakazi hao wa Sumbawanga, alisema kupitia maandamano na mikutano ya hadhara inayofanywa na chama hicho nchi nzima, CHADEMA imedhamiria kuamsha nguvu ya umma katika kuishinikiza serikali kupunguza kodi kwenye bidhaa na huduma muhimu ili bei zishuke na maisha ya wananchi yawe nafuu.
Alisema kupanda kwa gharama za maisha kumesababishwa na ufisadi na sera mbovu za serikali ya CCM, ambayo inawatoza kodi kubwa wananchi maskini kupitia bidhaa na huduma mbalimbali huku serikali hiyo hiyo ikiwasemehe kodi wawekezaji na wafanyabiashara wakubwa.
Katika hotuba yake hiyo iliyoonekana dhahiri kuwateka wakazi wa Sumbawanga, Mbowe alisema CHADEMA haipingi watu kulipa kodi, lakini haiko tayari kuona Watanzania maskini wakilipishwa kodi kubwa, huku serikali ikishindwa kuwapa maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Akifafanua zaidi historia ya kodi na athari zake kwa wananchi, kiongozi huyo wa kambi ya upinzani bungeni alisema baada ya serikali ya Rais Benjamin Mkapa kuondoa kodi ya maendeleo, ilileta kodi nyingine ya Ongezeko la Thamani (VAT), ambayo wananchi wote sasa wanatozwa kila wanaponunua bidhaa dukani na kulipia huduma mbalimbali kama usafiri.
“Nyerere alikuwa akikusanya kodi bilioni saba kwa mwezi, mzee Mwinyi aliondoka akiwa anakusanya kodi ya bilioni 27, akaja Mkapa yeye hadi anaondoka alikuwa anakusanya bilioni 300 na ushei. Baada ya hapo akaja Kikwete, yeye anakusanya bilioni 420 kwa mwezi. Anakusanya fedha nyingi kwa sababu kuna kodi ya VAT iliyoongezwa katika bei za bidhaa na huduma mnazolipia. Mnalipa kodi bila kujua, mnalipa kodi kwenye mafuta, kwenye soda, usafiri, sukari, sanda, pipi...kila kitu kodi kodi kodi,” alisema Mbowe na kuongeza.
“Kwa sababu ya kodi ya VAT, leo katika nchi hii kila mwananchi analipa kodi, mtoto, mjane, kijana, mwanafunzi wote wanalipa kodi …hadi maiti nazo zinalipiwa kodi mnaponunua sanda kwa ajili ya kuzikia. ...lakini kodi hizo zinaishia kustawisha maisha ya vigogo wa serikali, wananchi wa Sumbawanga na Watanzania wengine wanazidi kuwa maskini, mmefikia mahali hamuwezi hata kununua kilo moja ya sukari kwa ajili ya chai au kilo ya mafuta mnaanza kupimiwa kwenye vifuko vya shilingi mia moja...hali ya hatari hii, taifa lina msiba wa umaskini, wananchi wanalia kila mahali sasa, kila kona ya nchi,” alisema.
Akitoa mfano wa jinsi kodi inavyofanya bei za vitu kuwa juu, Mbowe alisema katika kila Sh elfu moja anayotumia Mtanzania kununua bidhaa sokoni au dukani au kulipia huduma, serikali humkata kodi ya wastani wa sh 500 hadi 600, kodi ambayo kama ikiondolewa gharama za maisha zitakuwa nafuu.
“Soda moja inapotoka kiwandani inapaswa kuuzwa kwa Sh 150 lakini kwa sababu ya kodi iliyowekwa na CCM kuanzia viwandani soda moja mnauziwa kwa sh 500 hadi 600. Kila mnaponunua mfuko mmoja wa cement mnakatwa kodi ya Sh 7,500 ambayo kama ikiondolewa au kupunguzwa bei ya saruji itakuwa nafuu na wengi mtaweza kujenga.
“Kila chupa moja ya bia unayonunua unakatwa kodi ya sh 800. Ndiyo maana Kikwete kwa mwezi anakusanya bilioni 420 kutoka kwenu, lakini maendeleo hakuna. CHADEMA tutakomaa na suala la gharama za maisha ndani na nje ya bunge mpaka Watanzania maisha yao yawe nafuu,” alisema Mbowe na kushangiliwa.
Katika mkutano huo pia Mbowe aliwahamasisha wakazi wa Sumbawanga kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kupata Katiba mpya na kushinikiza katiba hiyo itokane na wananchi na sio itokane kwa utashi na maamuzi ya Rais Kikwete kama ilivyopendekezwa katika Muswada wa Sheria ya Mapitio ya Katiba.
Naye Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe akiwahutubia wananchi hao alisema kwa nafasi yake kama Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi, ameagizwa na chama chake kuwasilisha bajeti mbadala katika bunge lijalo la bajeti ambayo pamoja na mambo mengine itashinikiza serikali kupunguza kodi kwenye mafuta ya petroli na dizeli kwa asilimia 50 ili yauzwe kwa angalau Shs 1665 kwa lita kutoka kwenye bei ya zaidi ya sh 2000 ya sasa.
“Gharama za maisha ziko juu kwa sababu ya mfumuko wa bei za mafuta ambao unasababisha na kodi. Bei ya mafuta ikishuka hadi 1,665 gharama za usafiri na bei za sukari na vyakula nazo zitakuwa angalau. Tutawataka waondoe kodi kwenye mafuta halafu wapunguze misahamaha ya kodi wanayoitoa kwa wawekezaji na wafanyabiashara wakubwa … serikali inasemehe bilioni 635 za kodi zinazopaswa kulipwa na matajiri, sasa hizo zikafidie kwenye mafuta baada ya kupunguza kodi. Wakikataa watakiona cha moto, tutafanya maandamano ndani na nje ya bunge mpaka kieleweke,” alisema Zitto.